Category: Jamvi la Kiswahili

  • ANGELLA OKUTOYI ASHINDA MASHINDANO YA WIMBLEDON

    (Picha kwa hisani ya The Standard)

    Na Gertrude Prosper

     

    Mchezaji wa tenisi, Angella Okutoyi mwenye umri wa miaka kumi na minane aibuka kuwa mwanamke wa kwanza kutoka Kenya kushinda mashindano ya Wimbledon. Katika mashindano hayo ya fainali, Angella alikuwa akishirikiana na Mholanzi Rose Marie Nijkamp katika timu ya wanawake Julai 9, 2022.

    Baada ya kushindwa katika seti ya kwanza ya 3-6 Okutoyi pamoja na mchezaji mwenzake waliamua kujikakamua na kushinda seti ya pili. Wapinzani hao, Kayla Cross na Victoria Mboko walishindwa (11-9) dhidi ya Nijikamp na Okutoyi (3-6, 6-4).

    Angella amevunja rekodi na kuwa Mkenya wa kwanza kufika katika fainali , akishirikiana na mwenzake Rose Marie, baada ya kuwashinda wapinzani wao Nikola Daubenova kutoka Serbia na Circa Bagaric kutoka Kroeshia (6-3 6-4) katika nusu finali.

  • WAZIRI MKUU WA ZAMANI WA JAPAN, SHIZO ABE AFARIKI DUNIA.

    (Picha kwa hisani ya OneIndiaNews)

    Na Gertrude Prosper

     

    Waziri Mkuu wa zamani wa Japan, Shinzo Abe amefariki dunia baada ya kupigwa risasi akiwa katika kampeni za chama chake cha Liberal Democratic Party (LDP) kwenye uchaguzi wa wabunge katika mji wa Nara Magharibi mwa nchi hiyo.

    Abe amefariki dunia hospitalini baada ya kulazwa akiwa mahututi kufatiwa kupigwa risasi katika mashambulizi hayo. Katibu Mkuu wa nchi ya Japan, Hirokazu Matsuno pamoja na Waziri Mkuu Fumio Kishida wamesema hali ya Abe ilikuwa mbaya baada ya kupata shambulio la moyo.

    Mshambuliaji huyo ameshakamatwa na maafisa wa usalama na walinzi wa Abe muda mfupi baada ya shambulio hilo.

    Shinzo Abe ni kiongozi wa zamani wa Japan kutumikia nchi hio kwa muda mrefu zaidi kuliko mawaziri wakuu wengine wote nchini humo. Abe alizaliwa Septemba 21 1954 jijini Tokyo na alianza harakati za kisiasa 1993 alipoteuliwa kuwa mwakilishi wa baraza la juu la bunge kisha akateuliwa kuwa katibu mkuu wa baraza la mawaziri Septemba 2005 kabla ya kuja kuchukua nafasi ya urais wa chama chake cha Liberal Democratic Party (LDP) mwaka 2006. Abe anatoka kwenye familia ya kisiasa ambapo babu yake alikua Waziri wa nchi hio kwanzia mwaka 1957 hadi mwaka 1960 na baba yake alikua katibu mkuu wa baraza la mawaziri la nchi hiyo, cheo ambacho kinaonekana ni cha pili kwa ukubwa zaidi nchi humo. Abe alikua Waziri mkuu wa Japan akiwa na miaka hamsini na miwili mwaka 2006, kiongozi wa kwanza kijana kuchukua nafasi hiyo. Muhula wake wa kwanza madakarakani uliubikwa na majanga kutokana na matatizo yake ya kiafya na kumfanya ajiuzulu. Alirejea tena serekalini na kutumikia wadhifa wa Waziri Mkuu katika nchi ya Japan kutoka mwezi Disemba mwaka 2012 hadi mwezi Septemba mwaka 2020.

    Abe atakumbukwa kwa sera yake ya kiuchumi akijaribu kufufua uchumi wa Japan uliokua umedorora. Atakumbukwa pia kwa kuongeza bajeti ya ulinzi na kubadili sera ya kijeshi ya Japan iliyodumu kwa miaka sabini. Alipambana pia kuboresha mahusiano yake na China.

  • JULAI 7: SIKU YA KISWAHILI DUNIANI

    1. (Picha kwa hisani ya Mwanaspoti)

    Na Abdul Shaban

     

    Siku hii inalenga kukuza matumizi ya Lugha hiyo kama nguzo ya Umoja, Ustawi na Amani

    Kiswahili ni miongoni mwa Lugha zinazotumiwa zaidi Afrika, na kwa Mujibu wa Umoja wa Mataifa (UN) ni kati ya Lugha 10 zinazozungumzwa na watu wengi duniani, ikiwa na wazungumzaji zaidi ya Milioni 200

  • TETESI ZA SOKA ULAYA

    Na Abdul Shaban

     

    Nyota wa Ureno Cristiano Ronaldo

    Nyota wa Ureno Cristiano Ronaldo, 37, ameafiki haja ya Manchester United ya kusaini mkataba na mshambuliaji mpya. (Express)

     

    Mshambuliaji wa Manchester City Mbrazil Gabriel Jesus

    Tottenham wana matumaini ya kuwapiku mahasimu wao wa kaskazini mwa London Arsenal katika mbio za kumsaka mshambuliaji wa Manchester City Mbrazili Gabriel Jesus kwa ofa ya soka ya Championi Ligi . (Mirror)

     

    Raheem Sterling

    Mshambuliaji wa Manchester City na England Raheem Sterling, 27, amekuwa akiwauliza watu kuhusu maisha katika magharibi mwa London huku klabu ya Chelsea ikiwa na nia naye. (Athletic)

     

    Dau la awali la £21.5m kwa ajili ya Sterling limekataliwa. (Fabrizio Romano)

     

    Chelsea wanaweza pia kumuhitaji mlinzi wa Manchester City mwenye umri wa miaka 27- Mholanz Nathan Ake. (Telegraph, subscription required)

     

    Mshambuliaji wa Chelsea na Ubelgiji Romelu Lukaku

    Mshambuliaji wa Chelsea na Ubelgiji Romelu Lukaku, 29, yuko tayari kurejea katika Inter Milan kwa gharama ya mkopo wa £8.5m pamoja na marupurupu aliyokubaliwabaina ya klabu hizo. (Mail)

     

    Manchester United wanaangalia uwezekano wa kufanya dai jipya kwa ajili ya kiungo wa kati wa Barcelona na Uholanzi mwenye umri wa miaka 25 Frenkie de Jong. (Fabrizio Romano)

     

    Kiungo wa kati wa Wolves na Ureno Ruben Neves

    Kiungo wa kati wa Wolves na Ureno Ruben Neves, 25, yuko katika orordha ya Manchester United ya wachezaji inayoweza kusaini mkataba nao iwapo watashindwa kusaini mkataba na De Jong. (Fabrizio Romano, via givemesport)

     

    Newcastle wamepewa ofa ya fursa ya kusaini mkataba na mlinzi Mivory Coast Eric Bailly, 28, kutoka Manchester United. (Mirror)

     

    The Magpies pia wameambiwa kuwa ni lazima walipe £50m kusaini mkataba na winga wa Bayer Leverkusen na Ufaransa Moussa Diaby. (Sun)

     

    Meneja wa Uholanzi na meneja wa zamani wa Manchester United boss Louis van Gaal alihusika kwa sehemu katika kumzuwia mlinzi wa Ajax Mholanzi Jurrien Timber, 21, kuhamia Old Trafford. (Marcel van der Kraan, Sky Sports)

     

    Ajax wametenga euro milioni 40 (£34.3m) wanazotaka kuzitoza Sebastien Haller, huku Borussia Dortmund wakiwa na nia na mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 27- kutoka Ivory Coast. (90min)

     

    Sunderland, Huddersfield na Bristol City wameweka dau la nyongeza la have £1m kwa ajili ya kiungo wa kati Muingereza mwenye umri wa miaka 21 anayechezea klabu ya AFC Wimbledon Jack Rudoni. (Sun)

  • SAFARI YA UMAUTI

    Na Abdul Shaban

     

    Maradhi yamenisibu, hadi leo naugua,

    Sasa naona aibu, afya imenipotea,

    Naomba kwake Wahabu, kwa rehema za jalia,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Naumwa nakondeana, dawa haziwezi tibu,

    Na kula siwezi tena, ameshasema tabibu,

    Ndugu wanawaza sana, waketi nami karibu,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Nikitizama kushoto, kisha narudi kulia,

    Baba lamtoka jasho, mama naye analia,

    Kauli ni changamoto, kinywani imepotea,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Muda unakaribia, kwa dalili nilo nazo,

    Mauti yanifikia, hilo halina vikwazo,

    Naona amenijia, asohitaji mawazo,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Sakaratil mauti, nilikuwa nasikia,

    Kiu ndo hakikauki, hata maji ya dunia,

    Makosa hayajifuti, madogo nilodhania,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Siwezi tena kutubu, kwa makosa nilofanya,

    Nimekuwa kama bubu, kwa uzito wake kinywa,

    Mauti yaniadhibu, na roho ninapokonywa,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Taarifa zatolewa, wengi wanahuzunika,

    *”Kweli tumeondokewa,na mpendwa bila shaka”*

    Kitandani natolewa, uchafu unanitoka,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Ndugu zangu na rafiki, wote wanalialia,

    Na wengine wameketi, eti wananiombea,

    Du’a zao hazifiki, natamani waambia,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Wanatafutwa wajuzi, tayari kuandaliwa,

    Wanikosha kwa simanzi, na marashi kufushiwa,

    Tayari mekwisha kazi, nje sasa natolewa,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Simanzi imegubika, baada ya kutolewa,

    Madeni kutangazika, nadai na kudaiwa,

    Swafu witri zimefika, ninaanza kuswaliwa,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Mbiombio napelekwa, kaburini kufukiwa,

    Tayari nimeshazikwa, huku watu wahusiwa,

    Mimi nimeshachafukwa, kwa maswali ninopewa,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

     

    Tubuni tubuni jama, kaburi lina vituko,

    Hapa mbavu zimebanwa, natamani rudi huko,

    Walau kwa moja jema, muda tena ndo haupo,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Nashauri walimwengu, tupunguzeni machafu,

    Na tuweni wachamungu, tusimuudhi Raufu,

    Pepo pahala pa mungu, hawapelekwi wachafu,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

    Wanadamu jihadhari, tusije kuangamia,

    Tusifanye ya khatari, mola atuangalia,

    Tuiandae safari, mema tukisubiria,

    Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

     

  • ENYI VIJANA

    (Picha kwa hisani ya Owlcation.com)

    Na Abdul Shaban

     

    Tulisifu na kulitukuza jina lake siku zote

    Kwa maana anatupenda sisi sote

    Uwepo wake umedhihirika kote duniani

    Siku zote nuru za nguvu zake huonekana hata gizani

    Wakati wa furaha na majonzi na dhiki

    Yeye ndiye dereva wa maisha yetu

     

    Enyi vijana, njooni nyote kwake Jalali

    Yeye ndiye mweza wa yote na aliye halali

    Tujiepushe na yale yanayomchukiza

    Tuwe tayari tuitwapo kusikiza

    Yake masharti kuyafuatilia daima

    Ili maisha yetu yaweze kusimama hima

     

    Enyi vijana, tuwe chombo cha kueneza amani

    Ili mioyo ya wazee na kote duniani iwe na furaha isiyo na kifani

    Tujiepushe na yale yanayoeneza chuki

    Bali tulitengeneza chakula cha ujirani wema kama asali kwa nyuki

    Tupige magoti tusali kwa Mola tukiomba dua

    Kuwa kila siku tuweze kuvutia kama ua

     

    Enyi vijana, yakini tukumbuke tulikotoka

    Tubadilishe yetu mienendo ili tupate kuokoka

    Tusiwe na mioyo mizito ilijaa takataka

    Bali tuombe msamaha kwake Mola mkono wake wa kulia tutakaa

    Tuweze kusimama imara katika imani yetu

    Tukijua ya kwamba mola hujibu maombi yetu

    Na yule amwaminiye hawezi kumwacha ateseke kamwe.

  • KITU KIZITO

    (Picha kwa hisani ya Dreamstime.com)

    {Na Abdul Shaban}

     

    Nakumbuka siku hiyo, niliketi kitandani,

    Alikuja mbiyombiyo, akalala kifuani,

    Akiwa mwenye kiliyo, kama yuko msibani,

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    Kabla kumuuliza, tatizo ni kitu gani,

    Ambacho kinamliza, akatoka furahani,

    Akanambia sikiza, “ewe wangu wa hubani”

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    Na mimi sikupuuza, kulifanyia utani,

    Sauti nikapunguza, ya redio pale ndani,

    Akaanza kunijuza, ili kunitoa dhani,

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    Kwa sauti ya kuimba, kama chiriku mbugani,

    Ndipo akaanza amba, kimtiacho shidani,

    Kuwa eti! Ana mimba, ni yangu si ya fulani,

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    Sikusubiri apoe, ama afike mwishoni,

    Ikabidi niyatoe, niliyonayo moyoni,

    Nikaanza na mayoe, yalonijaa pomoni,

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    “Nyonda wangu taratibu, sikiza yangu maoni,

    Japo jambo la aibu, mimba isiyo ndoani,

    Kulea ninawajibu, usiwe mwenye sononi”

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    Kwangu ikawa aula, sote tukiwa rahani,

    Nikazidi saka hela, viwe havikosekani,

    Vizurizuri vyakula, matunda pale nyumbani,

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    Ikakatika miezi, kwa rehema za Manani,

    Nikiyatoa malezi, mzuri yenye thamani,

    Akabariki Menyezi, kujifungua mwendani,

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    Huku nikiwa na hamu, nikawasili gangoni,

    Mtoto nimfahamu, aliyetoka tumboni,

    Sikuamini dawamu, nilichoona machooni,

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    Ayi! Nilipata tabu, sijawahi maishaini,

    Nikaiona ajabu, mbaya isiyo mfani,

    Ati! Napewa mwarabu, na mie hatufanani,

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

     

    Tama naachia nibu, kuongeza sitamani,

    Nyonda hana la kujibu, anaomba samahani,

    Kwa haya yalonisibu, siwezi kutamakani,

    Hakika kitu kizito, kimenipiga kichwani.

  • Prof.Laban Ayiro azungumzia Elimu ya Utatuzi chuoni Daystar

    Na; Righa Sedellar

    Profesa Laban Ayiro – Naibu Chansela.

    Hivi leo katika makala ya Dau La Elimu na Frank Otieno kwenye runinga ya KTN, Naibu Chansela wa chuo kikuu cha Daystar,Profesa  Laban Ayiro pamwe na Mhadhiri wa chuo kikuu cha Moi,Profesa Violet  Naanyu  na Profesa Lukoye Atwoli wa chuo kikuu cha Aga Khan walichangia pakubwa katika mjadala wa Elimu Ya Utatuzi Masuala (Problem based learning) na kusisitiza kuwa, mfumo huu wa elimu una faida nyingi sana katika maisha ya mwanafunzi.

    Elimu ya utatuzi masuala ni mfumo wa elimu unaolenga kutengeneza binadamu  anayeweza  kutatua matatizo mbalimbali ya kijamii,anayeweza kujimudu maishani na mwenye maadlili yanayoweza kutegemewa nchini na ulimwenguni.

    Profesa  Laban Ayiro alisisitiza kuwa chuo kikuu cha Daystar kimeshachukua mkondo huu wa mafunzo na kusema,”Katika chuo cha Daystar  Walimu huwa wanaenda madarasani ,wanawapa wanafunzi maswali na kuwaaacha wajadiliane na kutatua matatizo mbalimbali kisha kusahihisha matokeo yao kwani  nia yetu ni kutoa wanafunzi walio kamili baada ya kumaliza masomo yao katika chuo kikuu cha Dasystar”.

    Vilevile,wenza wake Profesa Ayiro walisisitiza kuwa,mfumo huu wa elimu unaweza kuwa wa manufaa zaidi japo walimu  pamwe na serikali yetu ya Kenya itatilia mkazo na kuhakikisha kuwa mfumo huu wa elimu umetiliwa maanani na kila mwalimu kutumia mfumo huu kuwaelimisha wanafunzi vyuoni.

    Aidha ,jopo hili la wataalam wa Elimu lilisisitiza kuwa,kuna haja kubwa sana ya walimu kunolewa zaidi na kufunzwa mfumo mpya  wa elimu ili nao pia waweze kuwafunza wanafunzi vyuoni kwani walimu wa sasa walifunzwa mfumo tofauti wa enzi zao. Imekuwa changamoto kubwa sana kwa walimu hawa kuwafunza wanafunzi kutumia huu mfumo mpya wa elimu.Fauka ya hayo,Profesa Violet Naanyu  alisisitiza kuwa elimu huwa ni safari  kwani huwa kuna mwanzo na huwa kuna lengo kuu la mwanafunzi anaposoma na mwalimu anapofunza. Kwa hiyo,Violet alilonga kuwa kuna umuhimu wa walimu kuwa na ushirikiano na wanafunzi ili pamoja waweze kukamilisha ‘safari’ ya  elimu aisee! Kidole kimoja hakivunji chawa .

    Kaditama,wataalam hawa walitoa maoni yao na kusema kuwa ,japo tunataka mfumo huu wa elimu kutufaidi ifaavyo, itabidi viongozi wa vyuo wafunzwe mbinu mpya ya uongozi. Viongozi wawe wanaokubali maendeleo na kuhakikisha kuwa maendeleo tofauti yanatekelezwa katika vyuo wanavyosimamia.

    Wakufunzi nao  wawe tayari kujadiliana na kukosoana na wanafunzi wasiwe na akili ya kufikiri kuwa ni wao pekee wanaojua yote. Wanafunzi pia walihimizwa kuwa na bidii za mchwa na wawe watu wa kutaka kujua mengi, wafanye utafiti na kutumia utafiti huo kutatua matatizo mbalimbali.

    Kwa uhahika,mjadala huu ulikuwa na mafunzo chungu  nzima na ni ombi langu kuwa wewe kama msomaji wangu utaweza kuyatilia maanani yaliyosemwa na wataalam na kuhakikisha kuwa, polepole  na kwa uhakika unakubali mfumo mpya wa elimu kwani mfumo huu una manufaa kadha wa kadha.

  • SIKUKUU YA MOI YAREJESHWA TENA

    Picha kwa hisani ya: businesstoday.co.ke

    Na Gladys Sheila,
    gladyshila52@gmail.com

    Katibu wa baraza la mawaziri katika wizara ya mambo ya ndani na uratibu wa serikali ya kitaifa Daktari Fred Matiang’i alitoa taarifa siku ya Jumanne na kuidhinisha sikukuu ya Moi kama sikukuu ya kitaifa.

    Hii ni baada ya uamuzi wa mahakama. Mnamo mwaka wa 2010, sikukuu ya Moi iliondolewa katika orodha ya sikukuu za kimataifa wakati katiba mpya ilizinduliwa rasmi. Mwezi wa Novemba mwaka wa 2017, jaji wa mahakama kuu alipinga uamuzi huo kwa kusema kuwa ni jambo ambalo linakiuka sheria. Mojawapo ya sababu ilikuwa kuwa sikukuu ya Moi haikuwa ya kuadhimisha wananchi au ufanisi wa nchi, bali mtu mmoja.

    “Kulingana na sheria kuhusu Sikukuu (Sura ya 110, Sheria za Kenya) na uamuzi wa mahakama katika Kesi ya Kikatiba Nambari 292 ya 2017, ninatangaza kuwa Oktoba 10, 2019, itakuwa sikukuu ya kitaifa,” Waziri Fred Matiang’i akasema.

    Hata hivyo, Wakenya wengi walikuwa na njia anuwai za kusherehekea siku hiyo. Wengine waliendeleza biashara zao kama kawaida, wengine wakisafiri kukutana na jamaa na familia zao na wengine wakapumzika kutoka kazini.

    Liliofanya sikukuu hii iwe ya kipekee ni kuwa wakenya wengi walitumia muda huu kuwatembelea na kuwapa msaada watoto katika nyumba za mayatima, wajane, wazee waliotengwa na familia zao, walemavu na wengineo kama ishara ya upendo.

    Hali kadhalika, wakenya wengine walikuwa na msimamo tofauti kuhusu maadhinisho ya sikukuu hiyo huku wakifananisha kipindi cha uongozi wa Mheshimiwa Moi kama dikteta.

    Picha kwa hisani ya: Nairobinews.nation.co.ke

  • MCHUANO WA KUKATA NA SHOKA

    Na: Dorothy Waweru
    dorothywaweru161706@daystar.ac.ke

    Picha: Wachezaji wakijikakamua uwanjani

    Sikukuu ya Moi chuoni Daystar ilisherehekewa kwa mbwembwe, vifijo na nderemo kwani katika uga wa “Santiago Barna Betheli” kama unavyojulikana na wacheza kandanda wengi, mchuano mkubwa ulikuwa ukiendelea. Mchuano huo uliandaliwa na wanafunzi wacheza kandanda ikiwemo; Walter Nalwa, Nicholas Atulo Snr, Cedrick na Dadiseh Olwaga ambao walinuia kujiburudisha katika mchezo huo wa miguu.

    Mchuano huo ulijumuisha timu sita zikiwemo: Blueboys, Rawa, Buffoons, Bomboclats, DCF handball na Fimbu. Timu hizi zilimenyana vilivyo ili kushinda zawadi murwa ambayo ilikuwa ni mbuzi mzima. Timu za Buffoons na Rawa ndizo zilifungua uga huo ambao ulikuwa na utelezi kufuatia mvua kubwa iliyokuwa imenyesha usiku wote.

    Timu ya Buffoons ilijikakamua katika dakika za kwanza huku Caleb Msando akiifungia timu hiyo bao la kwanza naye Nicholas Atulo Snr akifunga bao lao la pili. Timu ya Rawa ilijikakamua katika kipindi cha lala salama ambapo John Lemaiyan aliifungia Rawa bao lao la kwanza. Kitengo hicho cha kwanza cha mchezo kilipotamatika, Buffoons walikuwa wamefunga mabao mawili kwa moja.

    Mashabiki wa timu ya Buffoons walijaa uwanjani wakiimba nyimbo za ushindi kwani timu hiyo ingemchinja mbuzi kama zawadi ya ufanisi wao iwapo wangewashinda wenzao kwenye semifinali. Baada ya dakika chache za mapumziko, timu ya DCF handball ilijitosa uwanjani kumenyana na wachezaji wa timu ya Fimbu. Uzoefu mkuu katika mpira wa mikono wa timu ya DCF handball ulionekana kuwapa mkono uwanjani. Hata hivyo baada ya dakika kumi na tano Wallace kutoka timu ya Fimbu alifunga bao la kwanza. Baada ya dakika zingine tano, DCF handball ilisawazisha kupitia mchezaji Ephantus.

    Baada ya nusu wakati wa mchezo huo, timu ya Fimbu ilifunga bao lingine ambalo liliwawezesha kuibuka washindi katika kitengo hicho kwa mabao mawili kwa moja. Timu ya Blueboys vilevile ilichuana na timu ya Rawa huku wakifunga bao lao la kwanza ambalo lilikuwa la pekee katika mchezo huo hivi basi kuibuka washindi dhidi ya Rawa.

    Hata ingawa jua lilikuwa mtikati, wachezaji wa Bomboclat waliingia ugani kumenyana na DCF handball. Yasemekana kuwa wachezaji wa Bomboclat walikuwa wamekesha wakijitayarisha kwa mchuano huo wa kipekee. Katika dakika za kwanza, Bomboclat ilifunga bao lao la kwanza na baadaye kufunga la pili. DCF handball ilijizolea nunge hivi basi Bomboclat kuibuka washindi.

    Isitoshe, kabla ya semi fainali, Bomboclat ilichuana na Fimbu na wakailaza Fimbu bao moja kwa nunge. Timu zilizofuzu kwenye semi fainali ni Fimbu, Buffoons, Bomboclat na Blueboys. Mechi ya kwanza katika semi fainali ilikuwa kati ya Buffoons na Fimbu. Buffoons walilazwa bao moja la kufunga virago baada ya kucheza kwa ukakamavu mwingi sana.

    Nyuso za wachezaji wa timu ya Buffoons zilijaa simanzi kwani mbuzi alikuwa amewakwepa. Lisilobudi hubidi, Buffoons walidondolewa kwenye mchuano wakabaki kuwa mashabiki tu. “Ni uchungu sana mama kubeba mimba tumboni kwa miezi tisa halafu anampoteza mwana wake. Nasikitika sana kuwa tumeshindwa,” Duncan Olile, kipa wa timu ya Buffoons alisema.

    Timu za Bomboclat na Blueboys zilichuana kwenye mchezo wa pili katika semi fainali huku Bomboclat ikiibuka mshindi baada ya kuilaza Blueboys mabao mawili kwa nunge. Washindi wa semi fainali walikuwa Bomboclat na Fimbu. Wakati ukiwa saa kumi na mbili kamili, mchuano kati ya timu hizi mbili ulianza huku Bomboclat ikifunga mabao mawili mida ya dakika za kumi na tano za kwanza. Japo Fimbu iling’ang’ana kiudi na uvumba kujizolea angalau bao moja, jitihada zao hazikuzaa matunda kwani katika kipindi cha pili cha mchezo huo, Bomboclat ilifunga bao lingine. Bomboclat wakafunga mabao matatu kwa nunge.

    Mbwembwe na shamrashamra zilijaa uwanjani wakati ambapo wachezaji wa Bomboclat walipokabidhiwa mbuzi wao. Wachezaji waliachwa ugani wakisherehekea ushindi wao huku mashabiki wakiungana nao kushangilia ushindi wao.