Category: Jamvi la Kiswahili

  • MKAHAWA WA NDANI

    Na Chelangat Caren

    Maktaba ya chuo kikuu usiku ni ulimwengu mwingine kabisa, tofauti na shamrashamra za mchana. Giza la nje huongeza ukimya wa ndani, na taa zinazong’aa juu ya meza huangazia sura za wanafunzi waliojikita katika vitabu vyao au kompyuta zao ndogo. Hapa ndipo ndoto huwindwa kwa bidii isiyo kifani, kwa kikombe cha kahawa.
    Katikati ya mihadhara mizito na msongamano wa maktaba, kila mwanafunzi anahitaji kimbilio. Mahali pa kupumzisha akili, kunywea kahawa au chai moto, na labda kukamata kipande cha keki. Lakini je, unajua siri iliyofichwa ndani ya kampasi yetu ambayo inakupa yote haya, na zaidi? Tunanong’ona kuhusu ‘Mkahawa wa Ndani’.
    Huu si mkahawa wa kawaida; ni kama maktaba ndogo yenye harufu ya kahawa na vitabu. Ukuta mmoja umejaa rafu za vitabu vya zamani, vikiwa vimeachwa na wanafunzi waliomaliza masomo. Unaweza kukuta riwaya ya E. Kezilahabi, kitabu cha historia ya Kenya, au hata kitabu cha kuandaa maakuli . Wakati unasubiri kahawa yako, unaweza kupiga jicho kitabu chochote, na ukikipenda, unaweza kukichukua na kukiacha kingine chako. Ni mfumo wa kubadilishana vitabu usio rasmi lakini wenye roho.
    Mkahawa wa Ndani umekuwa ukumbi wa mikutano ya vikundi vya masomo, mahali pa mikutano ya ‘dating’ za kwanza zisizo na presha, na hata mahali pa kulia peke yako ukifurahia amani. zao zimetulia kuendana na bajeti ya mwanafunzi, na huduma yao ni ya kindugu. Ni zaidi ya mkahawa; ni moyo mdogo wa jumuiya yetu, unaotoa joto, maarifa, na nafasi ya kupumua. Nenda uujionee mwenyewe – labda utapata kitabu cha maisha yako, au rafiki mpya.
    Katikati ya mihadhara mizito na msongamano wa maktaba, kila mwanafunzi anahitaji kimbilio. Mahali pa kupumzisha akili, kunywea kahawa au chai moto, na labda kukamata kipande cha keki. Lakini je, unajua siri iliyofichwa ndani ya kampasi yetu ambayo inakupa yote haya, na zaidi? Tunanong’ona kuhusu ‘Mkahawa wa Ndani’.
    Huu si mkahawa wa kawaida; ni kama maktaba ndogo yenye harufu ya kahawa na vitabu. Ukuta mmoja umejaa rafu za vitabu vya zamani, vikiwa vimeachwa na wanafunzi waliomaliza masomo. Unaweza kukuta riwaya ya E. Kezilahabi, kitabu cha historia ya Kenya, au hata kitabu cha kuandaa maakuli . Unaposubiri kahawa yako, unaweza kupiga jicho kitabu chochote, na ukikipenda, unaweza kukichukua na kukiacha kingine chako. Ni mfumo wa kubadilishana vitabu usio rasmi lakini wenye roho.
    Mkahawa wa Ndani umekuwa ukumbi wa mikutano ya vikundi vya masomo; mahali pa mikutano ya ‘dating’ za kwanza zisizo na presha, na hata mahali pa kulia peke yako ukifurahia amani. Zao zimetulia kuendana na bajeti ya mwanafunzi, na huduma yao ni ya kindugu. Ni zaidi ya mkahawa; ni moyo mdogo wa jumuiya yetu, unaotoa joto, maarifa, na nafasi ya kupumua. Nenda uujionee mwenyewe – labda utapata kitabu cha maisha yako, au rafiki mpya.

  • Vita vya Kutisha Sudan na Matokeo Yake

    Na Joe Aura, aurajoe6@gmail.com 

    Dunia iko wapi? Kwa nini msitusaidie? Hili ni swali la mama mmoja aliyenusurika katika machafuko ya Sudan, maneno aliyoyasema kwa majonzi huku machozi yakitiririka. Katika vita vya kuwania mamlaka kati ya Jeshi la Sudan (SAF) na kikosi cha kijeshi cha Rapid Support Forces (RSF), maisha ya mamilioni yamebadilika kwa njia zisizoelezeka, huku masuala muhimu yakiwa hayaripotiwi ipasavyo.

    Chanzo cha Mzozo

    Vita kati ya SAF na RSF vilianza Aprili 2023, vikisababisha vifo vya maelfu na kuwafurusha mamilioni ya watu kutoka makazi yao. Ingawa vyombo vya habari kama BBC Kiswahili vimeripoti matukio ya dhuluma kama ubakaji na ukatili, masuala mengine yanayochangia hali mbaya ya kibinadamu yameachwa bila kufafanuliwa kwa kina.

    Athari za Mazingira

    Ukame mkali na mafuriko hatari yameongeza changamoto kwa jamii za Sudan ambazo tayari zinakabiliwa na athari za vita. Mabadiliko ya tabianchi yanayozidi kuzorota yanasababisha uhaba wa maji na chakula, hali ambayo haizungumziwi kwa upana katika vyombo vya habari.

    Mgogoro wa Wakimbizi

    Zaidi ya watu milioni moja wamekimbilia Sudan Kusini, huku watu milioni 14 wakihamishwa ndani ya nchi. Maeneo yanayopokea wakimbizi yameelemewa na uhaba wa rasilimali, hali inayohitaji msaada wa dharura wa kimataifa.

    Changamoto za Misaada ya Kibinadamu

    Kupatikana kwa misaada ya kibinadamu ni changamoto kubwa kutokana na ukosefu wa usalama na vikwazo vya usafiri. Mashirika ya misaada kama Shirika la Chakula Duniani (WFP) yamekuwa yakijitahidi kupenya katika maeneo yaliyoathirika zaidi, lakini juhudi zao zimegonga mwamba mara kwa mara.

    Njaa na Ukame

    Hali ya njaa imefikia kiwango cha janga, huku watu zaidi ya milioni 25 wakiwa na njaa kali. Katika kambi za wakimbizi na maeneo ya vijijini, watoto wanakufa kwa utapiamlo, hali ambayo ni ya kusikitisha na isiyofaa kupuuzwa.

    Ukatili wa Kijinsia

    Katika mizozo kama huu, wanawake na watoto wamekuwa wahanga wakuu wa unyanyasaji wa kijinsia. Ripoti kutoka kwa mashirika kama Amnesty International zinaonyesha kuwa ubakaji na dhuluma zimeongezeka kwa kasi, lakini simulizi hizi bado zinasikika kwa nadra kwenye vyombo vikuu vya habari.

    Athari kwa Elimu na Vijana

    Shule nyingi zimefungwa, na mamilioni ya watoto wa Sudan wameachwa bila elimu. Licha ya changamoto hizo, vijana wa Sudan wanaonyesha uvumilivu na matumaini, wakiwa tayari kujenga upya nchi yao ikiwa dunia itaonyesha mshikamano wa dhati.

    Huku dunia ikitazama, simulizi nyingi za mateso ya watu wa Sudan zinaendelea kuachwa bila kusikika. Ingawa vyombo vya habari kama BBC Kiswahili vimeangazia sehemu ya mzozo huu, masuala kama athari za mazingira, changamoto za misaada, na ukosefu wa elimu yanahitaji sauti zaidi. Kilio cha watu wa Sudan kinabaki kuwa kilio cha matumaini, wakitarajia msaada wa kimataifa utakapowafikia.

    Je, tutaendelea kufumbia macho hali hii au tutasikiliza kilio chao?

     

  • CAF Yachelewesha TotalEnergies CHAN 2024 hadi Agosti 2025

    Joe Aura, aurajoe6@gmail.com

    CAF yasema inahitajika muda zaidi ili kukidhi viwango vya kimataifa vya uandaaji

    Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) lilitangaza tarehe 14 Januari 2025, kucheleweshwa kwa michuano ya TotalEnergies African Nations Championship (CHAN) 2024, ambayo ilikuwa imepangwa kufanyika Kenya, Tanzania, na Uganda, hadi Agosti 2025. Uamuzi huu ulifuata tathmini za wataalamu wa Teknolojia na Miundombinu wa CAF ambao walibaini kuwa inahitajika muda zaidi ili kuhakikisha miundombinu na vifaa vinakidhi viwango vya CAF.

    Rais wa CAF, Dkt. Patrice Motsepe, alisifu maendeleo yanayoendelea Kenya, Tanzania, na Uganda katika kujenga na kuboresha viwanja vya michezo, uwanja wa mazoezi, hoteli, hospitali, na vifaa vingine muhimu kwa ajili ya mashindano haya ya bara. “Ningependa kutoa shukrani zangu za dhati kwa Rais William Ruto wa Kenya, Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania, na Rais Yoweri Museveni wa Uganda kwa uongozi wao na kujitolea. Nina imani kuwa miundombinu itakidhi viwango vya CAF, kuhakikisha kuwa mashindano haya yatakuwa ya mafanikio Agosti 2025,” alieleza.

    Uamuzi wa CAF unaonyesha kujitolea kwao kuhakikisha uzoefu wa kipekee wa mashindano kwa wachezaji, mashabiki, na wadau. Tangazo hili linasisitiza umuhimu wa kuboresha miundombinu ili kuendana na maono ya CAF ya matukio ya michezo ya kiwango cha dunia barani Afrika.

    Wakati mashindano hayo yamepangiwa tena, droo inayosubiriwa kwa hamu ya TotalEnergies CHAN 2024 itafanyika kama ilivyopangwa Jumatano, Januari 15, 2025, saa 20:00 EAT huko Nairobi. Tukio hili litakuwa na jukumu la kuamua makundi ya mashindano, na kuanzisha mashindano ya kushangaza.

    CAF bado haijathibitisha tarehe kamili ya kuanza kwa mashindano yaliyopangwa upya lakini imethibitisha kwa mashabiki kuwa ratiba mpya itahakikisha maandalizi katika mataifa yote yanayoshirikiana.

    Mashabiki wa Kenya, licha ya timu yao ya taifa kuwekwa katika kundi gumu, bado wana matumaini na hamu ya kuonyesha uwezo wa Afrika Mashariki katika kuandaa mashindano na uwezo wa soka katika jukwaa la bara zima.

    Wakati mataifa haya matatu yakijitahidi kumaliza maandalizi, CHAN iliyoahirishwa inatarajiwa kuwa mashindano ya kukumbukwa, ikisherehekea roho ya soka la Afrika.

     

  • Mlipuko wa Virusi vya Marburg Nchini Tanzania

    Joe Aura, aurajoe6@gmail.com 

    Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametangaza mlipuko wa virusi vya Marburg wiki moja tu baada ya waziri wa afya kukanusha uwepo wa visa vyovyote.

    Kisa cha kwanza kilichothibitishwa cha virusi vya Marburg kiliripotiwa katika mkoa wa Kagera, kaskazini-magharibi mwa nchi, wakati wa mkutano na waandishi wa habari siku ya Jumatatu. Tangazo hili lilitolewa wiki moja baada ya Waziri wa Afya, Jenista Mhagama, kukanusha uwepo wa virusi hivyo nchini. Rais Samia alihakikishia umma kuwa serikali imeimarisha juhudi za kukabiliana na mlipuko huo, ikiwa ni pamoja na kutuma timu ya dharura kufuatilia na kushughulikia visa vinavyoshukiwa.

    Tishio la Virusi vya Marburg

    Shirika la Afya Duniani (WHO) liliripoti awali mlipuko ulioshukiwa mnamo Januari 14, likisema kulikuwa na visa tisa na vifo vinane katika mkoa wa Kagera. Hata hivyo, uchambuzi wa sampuli ulibainisha kuwa ni kisa kimoja pekee kilichothibitishwa, huku visa vingine 24 vilivyoshukiwa vikipatikana kuwa hasi.

    Virusi vya Marburg, vinavyosambazwa kwa binadamu kupitia popo wa matunda na kwa kugusana na majimaji ya mwili ya watu walioambukizwa, ni hatari sana. Dalili za ugonjwa huu ni pamoja na homa, maumivu ya misuli, kuhara, kutapika, na katika hali mbaya, kifo kutokana na kupoteza damu kupita kiasi. Kwa wastani, virusi hivi huua asilimia 50 ya walioambukizwa, ingawa hatari ya kimataifa inachukuliwa kuwa ya chini, kulingana na Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dk. Tedros Adhanom Ghebreyesus.

    Tanzania ilikumbwa na mlipuko wa Marburg hapo awali mnamo Machi 2023, ambao uliua watu sita katika wilaya ya Bukoba. Mlipuko wa sasa unasisitiza hitaji la ufuatiliaji madhubuti katika maeneo yenye hatari kubwa kama Kagera, ambayo ni kitovu cha usafiri kwa wasafiri kutoka nchi jirani zikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Uganda, Burundi, na Rwanda.

    Shirika la Afya la Umoja wa Afrika, Africa CDC, linaripoti zaidi ya watu 300 waliotambuliwa kwa uchunguzi, wakiwemo wafanyakazi wa afya 56. WHO inashauri kutozuia safari, ikisisitiza ushirikiano wa kimataifa ili kudhibiti mlipuko huo.

    Kenya Yachukua Hatua za Tahadhari

    Huku kisa cha Marburg kikithibitishwa Tanzania, Wizara ya Afya ya Kenya imeongeza umakini. Ingawa hakuna kisa chochote kilichoripotiwa Kenya, mamlaka zinaimarisha mifumo ya ufuatiliaji, kufanya tathmini ya utayari, na kuandaa mpango wa kina wa kukabiliana na ugonjwa wa Marburg (MVD). Wizara hiyo pia ilisisitiza umuhimu wa vifaa vya kujikinga (PPE) kwa wafanyakazi wa afya na wale wanaowatunza wagonjwa ili kuzuia maambukizi.

    Kenya inabakia macho kutokana na mienendo mingi ya kuvuka mipaka na Tanzania, huku ikijitahidi kulinda afya ya umma dhidi ya MVD.

     

     

    Marejeo

    • BBC News; Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan athibitisha mlipuko wa virusi vya Marburg

    • Standard; Kenya yachukua tahadhari baada ya virusi vya Marburg kuthibitishwa Tanzania – The Standard Health

     

  • Hongera Septemba

    Na Mariita,

    Muhula wa Septemba umejawa na matukio mbalimbali ikiwemo michezo ya Falcon, burudani, wiki ya maonyesho ya mila na desturi za Kiafrika, biashara, utandawazi, mkutano wa kukuza mambo ya nje na mahusiano ya kimataifa vilevile kuweka msingi wa ujenzi wa maskani ya wanachuo.

    Hatua hii muhimu ya kulishughulikia suala la maskani, imeibua hisia chanya kwani Naibu Chansela Prof. Ayiro na bodi ya chuo hiki, amefanikisha mchakato wa mradi huu kwa upesi. Kwingineko, mradi wa ujenzi wa Mama Musau- Shule ya Sheria, unazidi kunoga kwani ukitembea kwenye sehemu ya tukio la ufundi, utashibishwa na mizani ya waashi ilivyoimara. Ni wazi kwamba Imani ya wengi sasa imetiwa kwenye kiambo.

    Aidha, kuna hamu kubwa ya kutaka chuo hiki kuangazia mradi ambao wengi watauita ‘MAMA YAO’ kwani kiuhalisia, bila pingamizi na kwa ushawishi mkubwa; Chuo Cha Dayastar kinafahamika nchini na ukandani kama Chuo Cha Mawasiliano. Uvumi wa sifa zake ni kama mawimbi baharini, kuenea kwa ubora huu kumetikisa mashariki na kati. Kiukweli, shule ya mawasiliano imepeperusha bendera na kuwa kama kitambulisho kamili cha Chuo Cha Daystar.

    Kituo chetu cha Redio Ya Shine, mitabendi 99.9 kingali kinafanyiwa ukarabati na hayo ni maendeleo kwenye sekta ya mawasiliano. Zaidi, ingelikuwa bora mno ikiwa kituo cha televisheni, ambacho sio tu kwa kuleta programu mbalimbali zihusianazo na habari, burudani, kupeperusha ibada chuoni na matukio ya ukuaji, kingelipata sehemu mwafaka ambayo ni jengo la shule ya mawasiliano ili kufufua uwajibikaji kwa kutoa motisha na kuwapa kipaumbele wenye talanta mbalimbali.

    Safari ya maendeleo italazimu kila mmoja kujibidiisha ili kudumisha sura ya Chuo na maadili kama mojawapo ya changizo katika kuimarisha ubora wa masomo na uongozi tabithi. Muhula huu wa Septemba unazidi kufunua vyungu vya mabadiliko na vilevile kupekua kurasa za maendeleo mahali mahali.

     

  • Sikitiko la moyo

    Na Mariita Joshua 

    Langu sikitiko ni haja ya moyo,

    Moyo wenye kuvunjika na kuvunda,

    Makovu yangalipo kama alama ya utambulisho.

    Nisijafa ili nililiwe ila vikao naviona jinamizini,

    Furaha imenikoma ili wimbi la kiza litawale,

    Nani wakunipa mapendo ili mtima udunde?

    Mbona raha inikauke wakati chemichemi inabubujika?

    Nguvu sinazo, ni lelemama jina langu,

    Hawahitaji kwenda vichekeshoni,

    Mwenyewe ningalipo kitimbwi,

    Pembeni nimevikwa kirauni, mashaka mie!

    Kama matambara nimeraruka,

    Afadhali nipige deki matapishi yalozagaa sakafuni,

    Nikanyagwe na wenyeji kwa wageni,

    Nitumbukizwe majini niloe nifinyangwe.

    Wakila vitamu nilambishwe munyu,

    Niwe na ndia ndefu ya kuibusu asubuhi ifatayo,

    Nikorome kochini matumbo yakikohoa,

    Shadidi inikumbate nikauke kama aiskrimu.

    Niwe Kinyago kokote,

    Wa kuonwa niwe ila kusikiwa aa!

    Ninyate ili guu lisiporomoshe mwendo

    Nijambe ila lisinuke, niwe kimyaaa!

  • TUMBIRI BWALONI

    Na Mariita Joshua Ongoro

    Nimefika kwenye bwalo, nipo foleni nawaona wanachuo kila mtu kashika hamsini zake. Nina mkoba wangu wa ngozi umening’inia begani na kila ninapotembea, mkoba nao unacheza densi ya shwii shwaa. Mwanangu nakumbuka kipindi kile nilikuwa shule ya msingi kijijini Gusii; Mabonde na milima, nilishuka na kupanda nikiwa na kijikoba cheusi chenye mkanda wa mchungwa. Unaelewa jinsi mvua ikianza kunya, hasa pale kijijini, hamna pa kujikinga maana migomba ya ndizi kila sehemu. Itakubidi ukurupuke mbio huku mkoba nao unakucharaza makofi kwenye vilima vya mwili – yaani makalio. Kaptura nayo ina vijisehemu vya kuingizia hewa kwa jinsi ilivyoraruka na kuchakaa, utadhani sehemu ile ya nyuma ina macho. Ukishafika nyumbani baada ya kukurupuka ja Nyantika Maiyoro, mkimbiaji shupavu wa Gusii siku za nyuma, utadhani madaftari kahariwa kule nyuma kumbe unyevunyevu na harufu ya jasho nzito.

    Safari hii nimeepuka kuvaa kaptura ya aina yoyote na mkoba nimehakiki si wa mchungwa. Ingawaje ni mweusi, sasa ni wa ngozi, si wa nyuzi wala kitenge. Zamu yangu ya kuhudumiwa inatimia. “Nipe chai kwa maandazi halafu unitilie kayai kamoja.” Ninatamka bila ya kujali sarufi. Mbali na udunisho wa ‘kayai kamoja’ Inanikumbusha kuwa, ukienda Mwanza, basi utajutia kutohudumiwa unaposema ‘nipe’ kwani unamiliki wewe bidhaa hiyo? Tusiseme mengi maana hata salamu huja mwanzo. Je, Pwani yetu ya Kenya, maadili yamedumishwa ama vijana wameroga ufanisi huu kwa lugha za mitaani kama Shembeteng’ ya Jeshijinga? Kwanza hata kuwasikia leo imekuwa siwapati. Jamani nijibuni; Waliendapi Jeshijinga?

    Taratibu natembea nikikokota miguu kana kwamba nipo mwezini ili nisilambe sakafu kwa pupa zangu. Naangaza macho yangu kuelekea meza iliyo pembeni mwa mlango wa kuvukia kwenda sehemu ya pili ya bwalo hili. Natabasamu japo mwonekano huu utadhani ninalia ndo maana hata nikaambiwa eti sura yangu mimi inaweza kuwachekesha wagonjwa hospitalini wakavunja mbavu hadi kupona kwa jinsi ilivyojaa makunyanzi. Basi ninapunguza tabasamu hilo la kutisha ninapokumbuka maneno ya abu. Ninachongea mezani na kuchukua uma. Cha kushangaza ni kwamba sikufahamu kuwa baada ya kumiminiwa chai pale bwaloni, ni jukumu langu kujitilia sukari. Mimi naye ninaenda zangu mezani na ninaonja ile chai, Lo! “Mbona hawatii sukari bwanaaa? Hii chai bubu sasa…” Ninajinung’unikia kwa tafsiri ya mama- bubu ni kinywaji kisichokuwa na sukari kwenye lugha ya kisiri ya Gusii. Muda nao unakwenda sana. Siwezi kurudi ili nitie sukari maana hata nishazoe mimi. “Kwanza sukari ni sumu mwilini, ni vizuri kunywa ya namna hii maana ni afya hii.” Ninajishawishi.

    Punde tu nikiwa mjadalani, nasikia purukushani, viti vinasongasonga ovyoovyo. Ala! Hamna mtu bwaloni hasa upande huu wa chini. “Basi nini?” Ninakodoa macho upande wa kushoto nawaona tumbiri, mama yangu! Hivi, nitakunywa chai kweli ama nimewanunulia hawa wapumbavu? Tunaangaliana maana kila mmoja yuko chonjo. Kidogo tumbiri anaruka mezani. Mimi ni mwanaume siwezi kuchezewa shere hii. Ninanyanyua mkono na kuuchezesha kuelekea kwake yule mshenzi, kana kwamba ni nyoka anayeinda na huku usoni nimetia makunyanzi tishti.

    Ni kweli tumbili naye alihofia maisha yake mafupi ila hakuchoka. “Mimi kwanza ni mwanamme na tumbiri huwaogopa sana wanaume. Si nawaona jinsi wanavyowaangaisha wanadada chuoni zaidi ya wanaume.” Nikajitia nguvu. Upo wakati nilikuwa nikitokea zangu maabara ya kompyuta kule epada yaani EPD, kwa umbali nikawaona wanadada wamekongamana sehemu moja kijia-panda cha SBE. Nikawa sina habari ya lile kundi lililozubaa. Basi kwa mpito wangu nikiwa nimetangulia nawasikia nyuma yangu wamefuata. Ninashangaa. Kumbe mwanangu, wasichana wale walikuwa hawana mtu wa kuwavusha kwenye bahari shamu ya tumbiri waliofurika nje ya shule ya sheria. Basi nikawa Musa niongozaye huku nyuma yangu Waisraeli wamenifuata wakielekea ‘Kanani.’

    Kwenye idara ya Saikolojia, ipo nadharia inayoitwa; Uhamisho wa elimu ambayo kwa kimombo tunaita ‘transfer of knowledge’ ambayo hufundisha kwamba, mtu husuluhisha tatizo kutokana na kusoma yaliyotendeka nyumaye. Mimi kama mwanasaikolojia nilikumbuka kuwa hawa tumbiri huwaogopa wanaume. Basi, mimi ni nani? Lazima niwatishe hawa washenzi. Lakini haikuwa rahisi. Mezani ninaamua kupapia maandazi yale ili angalau nisitoke bilashi. Sasa siwezi kutumia uma kula kwa ustaarabu ila mikono. Upande mwingine namsikia tumbiri mvunguni mwa meza anatapatapa kwa kucha zake. Ninaanza kurusha mateke, “Mniache bwana.” Ila ninapomshtua basi anaruka mezani. Kwa ufundi huu wa kula ninasafisha sahani FYU na ninabakia na yai. Chai sijanywa. Ninachukua uma na kuanza kutoa maganda lakini siwezi maana nimekazwa sana. Naitumia mikono tena. Ninatafuna kipapachipapachi huku nikiangazaangaza macho utadhani naiba kula. “Basi mnyweni hiyo chai ‘bubu’ maana hata haina faida.” Ninakejeli nikijipangusa midomo kwa hanchifu yangu ya zambarau na madoadoa ya samawati. Nimeshinda vita maana hata chai hawakunywa.

     

  • STR8 UP YAALIKA KIZAZI CHA GEN Z

    Na Leeroy Wuone

    Wanafunzi wa chuo kikuu cha Daystar shule ya mawasiliano walihudhuria hafla iliyoandaliwa Standard group mnamo Jumamosi tarehe 28 Septemba mwaka wa 2024.Wanafunzi kumi na watatu walihudhuria hafla hio iliyobandikwa jina “Siku ya ubunifu ya kizazi cha Gen-Z’’.

    Lengo la Standard group la kuandaa hafla hio ilikuwa kuwahamasisha wanafunzi kuhusu mambo yanavyoendelea kwenye studio pale Standard group na ambavyo watu tofauti tofauti hushirikiana kila siku kuleta habari kemkem za hivi punde kila siku,zaidi ilikuwa siku ya kutangamana na wasanii kwenye sekta mbalimbali mfano ni anayejulikana kwa jina mluo_social.light ambaye alihudhuria hafla hiyo na kikosii chake ambao wametamba kwenye majukwaa ya mitandao ya kijamii kama Instagram na Tiktok.

    Aliyetuzungusha kwenye sakafu ya kwanza “ red carpet’’ alisema kuwa uchapishaji wa magazeti ndio ulikuwa mwanzo wa the standard group kisha ikaja enzi ya televisheni na baadaye habari kwneye mitandao ya kijamii.

    Kelly alipeana mfano akisema kwamba tuseme iwapo mwanahabari ametumwa kule CBK kwenye hafla ya uchapishaji wa noti mpya hawezi kuiweka taarifa hio mtandaoni bila kuwajulisha wahariri ambao wako kwenye chumba cha habari.

    Kupangwa kwa red carpet ulikuwa kimkakati ndiposa waandishi wa habari hao waweze kufanya kazi kwa kijumla ili kushinda ushindani.Alitujulisha kuwa zile tahadhari za kwanza za habari hutumwa kwenye “radar desk’’ kwenye kituo cha Standard group. Lengo lao pia ni kulisambaza habari vilivyo bila kuutia chumvi .

    “Checkpoint’’ ilikuwa katikati na hapo ndipo habari za kiteknolojia kama kilimo na hata mambo ya takwimu yalifanyiwa utafiti kabla habari kupeperushwa.Mfano wa takwimu ni kwa mfano idadi ya magari ambayo Wakenya hununua na magari yapi kwa idadi?

    Iwapo mwanahabari ana tashwishi na utafiki wake ya nambari ataelekea kwa wanaofanya hapo checkpoint kwa usaidizi mwafaka. Alizidisha kwa kusema iwapo wanaofanya hapo checkpoint wapokee hadithi yako kama mwanahabari,wanaweza kupa takwimu zaidi ambayo ni sahihi mno.

    Mwanafunzi mmoja aliuliza kuhusu watu ambao wanaendesha tarakimu zilizoandikwa kwenye runinga pale kwenye red carpet kisha alijibu ya kwamba kuna wasanidi wa wavuti ama ukipenda kwa kiingereza “web developers’’ ambao kazi yao ni kujumuisha idadi ya Wakenya wanaosoma taarifa za magazeti kwa siku moja.

    Mwishowe wageni walitumbuizwa na hata kucheza densi. Watu waliweza kujifunza mengi na hata kujenga mahusiano na wakubwa katika sekta ya mawasiliano.

     

  • HEKAHEKA ZA MUHULA WA SEPTEMBA

    Na Mariita Joshua Ongoro

    Ni kweli kwamba mihula ya masomo hapa chuoni huwa na mambo yanayochipuka mwanzoni, kati na hata mwishoni. Muhula ukianza kawaida kuna kule kung’ang’ana na hali ya ulipaji karo, usajili wa masomo na mahudhurio ya mara kwa mara. Zaidi, hamna jambo linalobubujisha msongo wa mawazo kama vile kukosa chumba cha kupanga. Je, ni wangapi huzurura kotekote, mapana na marefu, kujaribisha nasibu ya kupanga angalau hata mabatini? Wakati mwingine huambulia patupu kwa kusononeshwa na kauli za wasimamizi wa vyumba vya kupanga, “Hamna chumba labda ujaribishe huko Portland.” Tabu. “ Ama kama hutojali, kunacho chumba pembeni kuleee… hakina umeme ila baadhi ya wenzenu wameshawahi kuishi siku za nyumba hali hii ilipojitokeza.” Utamsikia akiongeza kwa kutojali kana kwamba ni jeuri.

    Mbanano wa wanachuo nje ya shule imeleta hali chanya na pia hasi. Vyumba vya kupanga kila sehemu vimebeba mamia ya wanachuo na ni dhahiri kwamba wamiliki wa vyumba hivyo, hawajajutia ujenzi wao japo uliwagharimu kiasi kikubwa cha fedha. Kwa upande mwingine, uhitaji wa upangaji umeibua mijadala na hisia tofautitofauti kuhusu ongezo la kodi. Vyumba ni vile vile, hali ni ile ile, wanafunzi ni wale wale, maji ni yale yale tena ya chumvi; itakuwaje kuongeza kodi hata muda hamna vyumba vya kupanga? Sarakasi hii, pengine inawafaidi pakubwa wasimamizi hata kupita wamiliki halisi.

    Uhalisia wa elimu ya chuo inafafanuliwa kivipi? Je, kuna namna inayoweza kujitokeza ili iwe suluhisho kwa misukosuko na mawimbi ya jinsi hii? Cha kusikitisha ni kwamba, jinsi ujio wa wanachuo unazidi kunoga, basi hali hii inazidi kuyumbisha matamanio. Ingawaje kuna mahafali wa kila mwaka, wanaoingia huzidi mtoko. Sintofahamu inayopeperusha bendera miongoni mwa wanachuo ni kwamba chuo hiki, kwa jinsi kinavyofahamika kwa sifa zake, je, haingekuwa dhahiri kuwekeza katika miradi inayowanufaisha wanafunzi maana hawa ndio walengwa wakuu?

    Hatuwezi kulifumbia macho suala la Naibu Chansela, Prof. Ayiro kuchakatua miradi ya maendeleo kila baada ya muhula ama tuseme kila siku. Ni wazi bila pingamizi kuwa kati ya wazalendo na wachapakazi wa kweli, basi Profesa Ayiro amevikwa taji kwani ni mmoja wao na pengine kiongozi wao. Lakini mojawapo ya wasilisho la ombi kuu ambalo lingehitaji uchambuzi ni hili: Ujengaji wa vyumba vya malazi kwenye ardhi ya chuo hiki.

    Umuhimu wa ujenzi wa vyumba hivi ni pamoja na kodi inayoweza kugharamiwa na wanachuo hata wa kiwango cha chini. Ukengeufu uliopo kwenye mazingira ya nje ya shule ni pamoja na ukosefu wa maji, maji yasiyo safi kwa hali ya kutotibiwa mfano kwa njia ya klorini. Ukuaji wa chuo hiki kunategemewa na vizazi kwa sababu kutawafaidi waliomo na wasiokuwemo. Hivi sasa wanachuo wanazidi kukumbwa na hali ya kumudu maisha na pia utekelezaji wa majukumu yao kama vile kufika chuoni kwa wakati, kutimiza maono na lengo la elimu. Ladha ya kufanikisha vipengele vyote muhimu itatiwa kwa kulainishwa kwa masuala tata kama haya ya upungufu wa vyumba vya kupanga. Hekaheka za Septemba zahitaji hali kutengemaa.

  • Matukio na Matokeo Ligi Kuu Nchini Uingereza

    {Picha kwa hisani MyBroadBand}

     

    Na Dennis Mungai

     

    Raundi ya nne ya mechi Ligi kuu nchini Uingereza imekamilika wikendi hii siku ya Jumapili, mechi ya mwisho ikiwa baina ya  Arsenal dhidi ya Manchester United. Mechi yenyewe ilikua ya kusisimua, The Gunners wakipata ushindi wa mabao tatu kwa moja. Declan Rice alifunga bao lake la kwanza kama mchezaji wa Arsenal kisha Gabriel Jesus kufunga la tatu na kuhakikisha ushindi wao. Bao la United lilifungwa na Marcus Rashford kisha Martin Odegaard kusawazisha dakika moja baadaye. Vijana wa Erik Ten Hag sasa wapo katika nafasi ya kumi na moja wakiwa na alama sita huku Arsenal wakiwa na alama kumi.

    Siku ya Jumamosi ilishuhudia wachezaji watatu wakifunga mabao matatu kila moja, ama kwa Kimombo “hat-trick”. Evan Ferguson wa Brighton alifunga mabao matatu kusaidia timu yake kupiga Newcastle 3-1. Erling Haaland alifunga mabao matatu pia na kuzalisha lingine huku vijana wa Pep wakigaragaza Fulham 5-1. Mabao mengine yalifungwa na Nathan Ake na Julian Alvarez. Spurs walishinda Burnley 5-2, Son Heung-Min akicheka na wavu mara tatu huku Romero na James Maddison wakiongezea vijana wa Vincent Kompany masaibu baada ya kupandishwa daraja msimu huu.

    Jurgen Klopp alipata ushindi wa 3-0 katika mechi yake ya mia tatu kama mkufunzi wa Liverpool.  Szoboszlai na Salah walifungia Reds huku difenda wa Aston Villa Matty Cash akijifunga. Crystal Palace walipata ushindi wa mabao matatu kwa mawili dhidi ya Wolves nayo Chelsea walilazwa 1-0 na Nottingham Forest.

    Siku ya Ijumaa West Ham walishinda Luton Town mabao mawili kwa moja, Jarrod Bowen akiendeleza msururu wake wa  kufunga mabao msimu huu. Brentford na Bournemouth walitoka sare ya mabao mawili nayo mechi ya Sheffield United na Everton kumalizika kwa matokeo sawia.  Ligi itachukua mapumziko ya mechi za kitaifa za kirafiki na itaendelea tarehe kumi na sita mwezi huu.