Category: Michezo

  • CAF Yachelewesha TotalEnergies CHAN 2024 hadi Agosti 2025

    Joe Aura, aurajoe6@gmail.com

    CAF yasema inahitajika muda zaidi ili kukidhi viwango vya kimataifa vya uandaaji

    Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) lilitangaza tarehe 14 Januari 2025, kucheleweshwa kwa michuano ya TotalEnergies African Nations Championship (CHAN) 2024, ambayo ilikuwa imepangwa kufanyika Kenya, Tanzania, na Uganda, hadi Agosti 2025. Uamuzi huu ulifuata tathmini za wataalamu wa Teknolojia na Miundombinu wa CAF ambao walibaini kuwa inahitajika muda zaidi ili kuhakikisha miundombinu na vifaa vinakidhi viwango vya CAF.

    Rais wa CAF, Dkt. Patrice Motsepe, alisifu maendeleo yanayoendelea Kenya, Tanzania, na Uganda katika kujenga na kuboresha viwanja vya michezo, uwanja wa mazoezi, hoteli, hospitali, na vifaa vingine muhimu kwa ajili ya mashindano haya ya bara. “Ningependa kutoa shukrani zangu za dhati kwa Rais William Ruto wa Kenya, Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania, na Rais Yoweri Museveni wa Uganda kwa uongozi wao na kujitolea. Nina imani kuwa miundombinu itakidhi viwango vya CAF, kuhakikisha kuwa mashindano haya yatakuwa ya mafanikio Agosti 2025,” alieleza.

    Uamuzi wa CAF unaonyesha kujitolea kwao kuhakikisha uzoefu wa kipekee wa mashindano kwa wachezaji, mashabiki, na wadau. Tangazo hili linasisitiza umuhimu wa kuboresha miundombinu ili kuendana na maono ya CAF ya matukio ya michezo ya kiwango cha dunia barani Afrika.

    Wakati mashindano hayo yamepangiwa tena, droo inayosubiriwa kwa hamu ya TotalEnergies CHAN 2024 itafanyika kama ilivyopangwa Jumatano, Januari 15, 2025, saa 20:00 EAT huko Nairobi. Tukio hili litakuwa na jukumu la kuamua makundi ya mashindano, na kuanzisha mashindano ya kushangaza.

    CAF bado haijathibitisha tarehe kamili ya kuanza kwa mashindano yaliyopangwa upya lakini imethibitisha kwa mashabiki kuwa ratiba mpya itahakikisha maandalizi katika mataifa yote yanayoshirikiana.

    Mashabiki wa Kenya, licha ya timu yao ya taifa kuwekwa katika kundi gumu, bado wana matumaini na hamu ya kuonyesha uwezo wa Afrika Mashariki katika kuandaa mashindano na uwezo wa soka katika jukwaa la bara zima.

    Wakati mataifa haya matatu yakijitahidi kumaliza maandalizi, CHAN iliyoahirishwa inatarajiwa kuwa mashindano ya kukumbukwa, ikisherehekea roho ya soka la Afrika.

     

  • Matokeo na matukio Ligi Kuu Uingereza

     

    Na Dennis Mungai

     

    Raundi ya kumi na sita za mechi ligi kuu nchini Uingereza ilikamilika jana usiku baada ya mechi baina ya Liverpool na Manchester United. Mechi hiyo ilitoka sare tasa huku vijana wa Erik Ten Hag wakiweka ulinzi uliokua mgumu kupitwa na mashambulizi ya Liverpool. Diogo Dalot wa United alipewa kadi nyekundu katika dakika za mwisho lakini bado vijana wa Klopp hawakupata nafasi ya kufunga bao. Matokeo hayo yanawaacha Liverpool katika nafasi ya pili nayo United kushuka mpaka nafasi ya saba.

    Kwingineko, Arsenal walimaliza wikendi katika nafasi ya kwanza katika jedwali baada ya kuipiga Brighton 2-0. Mabao ya Jesus na Havertz yaliipa timu yao alama tatu kabla ya kumenyama na Liverpool siku ya Jumamosi. West Ham waliiduwaza Wolves 3-0 nayo Aston Villa iliendeleza msururu wa matokeo mazuri kwa kuipiku Brentford 2-1.

    Siku ya Jumamosi,  Chelsea ilishinda Sheffield United 2-0, huku mchezaji mpya Christopher Nkunku akirudi kikosini ila hakucheza mechi hiyo. Newcastle walizidi nguvu Fulham baada ya kutolewa katika mashindano ya  ligi kuu ya Mabingwa Ulaya, vijana wa Eddie Howe wakipata ushindi wa mabao tatu bila jibu. Everton walipiga Burnley mabao mawili kwa bila nayo Spurs kuilemea Nottingham Forest kwa matokeo sawia siku ya Ijumaa.

    Mabingwa watetezi Man City walipoteza alama nyingine baada ya kutoka sare ya mabao mawili dhidi ya Crystal Palace. Grealish na Rico Lewis waliipa City uongozi lakini Mateta na Olise walifunga katika dakika za mwisho kujinyakulia alama moja. City sasa wapo katika nafasi ya nne kabla ya kuenda nchini Saudi Arabia kucheza michuano za FIFA Club World Cup.

  • Matokeo ya Ligi Kuu Uingereza

    Mpambano wa Stamford Bridge kati ya Chelsea na Manchester City ulichipuka kama gari la burudani lililowacha mashabiki bila pumzi baada ya tamasha.

    Mchezo ulichukua muda kuanza, na Erling Haaland akifungua mlango kwa City katika dakika ya 25 kutoka kwa kipindi baada ya mzozo na Cucurella.

    Chelsea ilijibu haraka, na kichwa cha nguvu cha Thiago Silva kusawazisha na Raheem Sterling kufunga dhidi ya timu yake ya zamani, kuwaweka wenyeji mbele 2-1.

    City, hata hivyo, iliendelea kuonyesha upinzani, kichwa cha Akanji likipita lango kulirudisha mchezo sare ya 2-2.

    Mzunguko uliendelea Haaland akifunga bao lake la pili, kupeleka mabingwa mbele kwa 3-2.

    Chelsea, bila kutoa mwanya wa kushindwa, ilijibu kupitia Jackson, kufanya mabao kuwa matatu kwa kila upande.

    Mchezo ilifikia kilele chake wakati Rodri inavyoonekana akif unga bao la ushindi kwa City na dakika nne zilizosalia, akichukua fursa ya kugonga kubwa kutoka kwa Thiago Silva. Lakini, kwa kugeuka kushangaza, Broja wa Chelsea aliibuka kuwa shujaa aliposhinda mkwaju wa penalti baada ya kuchezewa vibaya na Dias.

    Katika kugeuka kwa kuvutia, Palmer, mchezaji wa City msimu uliopita, alijitokeza kuchukua penalti, kuhakikisha sare ya 4-4 .

    Matokeo haya yaliisukuma Chelsea juu kwenye nusu ya juu, kuandaa jukwaa kwa pambano linalosubiriwa kwa hamu na Newcastle United baada ya m apumziko ya kimataifa.

    City, kwa upande mwingine, ilikosa nafasi ya kuongeza uongozi wao kileleni na sasa inakabiliana na mchezo mkubwa nyumbani dhidi ya Liverpool katika mechi zijazo.

  • Matokeo ya Ligi kuu Nchini Uingereza

    Na Denni Mungai

    Manchester City walipata ushindi wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Brighton siku ya Jumamosi. Julian Alvarez alifunga bao la kwanza naye Erling Haaland alifunga bao lake la tisa msimu huu kuipa City uongozi katika kipindi cha kwanza. Ansu Fati alifunga bao lake la kwanza kama mchezaji wa Brighton lakini haikutosha kupata alama katika uwanja wa Etihad.

    Katika mechi nyingine, Brentford waliipiga Burnley 3-0, Newcastle kuiduwaza Crystal Palace 4-0 nayo Wolves kupata ushindi wa karibu wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Bournemouth. Mechi kubwa ya wikendi kati ya Chelsea na Arsenal iliisha sare ya mabao mawili. Chelsea ilikua inaongoza kwa mabao mawili lakini Declan Rice na Leandro Trossard walisawazisha na kusaidia timu yao kunyakua alama moja. Vijana wa Arteta bado hawajashindwa kutoka msimu uanze na wana alama 21 baada ya mechi tisa.

    Man United waliipiku Sheffield United 2-1, mabao ya United yakifungwa na Mctominay na Diogo Dalot. Mohamed Salah alifunga mabao mawili na kusaidia timu ya Liverpool kushinda Everton 2-0 katika mechi ya kwanza siku ya Jumamosi. Siku ya Jumapili, Aston Villa waliigaragaza West Ham 4-1. Douglas Luiz alifunga mabao mawili huku Ollie Watkins akifunga bao lake la tano msimu huu. Leon Bailey alitia kimiani bao la nne na kusaidia Villa kupanda mpaka nafasi ya tano katika jedwali.

    Tottenham Hotspurs walirudi kileleni mwa jedwali baada ya kuishinda Fulham 2-0. Son Heung-Min na James Maddison waliifungia timu yao na kuiipa alama tatu. Spurs wana alama mbili zaidi ya Man City, walio katika nafasi ya pili. Timu ya Postecoglou wana nafasi ya kuzidisha pengo hilo watakapocheza na Crystal Palace siku ya Ijumaa.

     

  • Ligi kuu ya mabingwa barani Ulaya

    (Picha kwa hisani ya SoccerBible)

     

    Na Dennis Mungai

    Raundi ya pili za mechi za makundi ligi ya mabingwa barani Ulaya itaendelea wiki hii. Siku ya Jumanne mechi nane zitachezwa, ya kwanza ikiwa kati ya Union Berlin na Braga ya Ureno. Vijana wa Erik ten Hag Manchester United wataialika Galatasaray huku wakitafuta ushindi wao wa kwanza katika kundi lao.

    Mabingwa watetezi wa ligi ya Italia Napoli watakua wenyeji wa Real Madrid nayo Arsenal itasafiri hadi Ufaransa kumenyana na Lens.  Copenhagen watachuana na Bayern Munich, Inter dhidi ya Benfica nayo PSV watacheza na Sevilla. RB Salzburg watakua wataialika Real Sociedad ya Uhispania.

    Siku ya Jumatano Borussia Dortmund watachuana na AC Milan huku Celtic wakipambana na Lazio. Baada ya miaka ishirini nje ya michuano hizi, Newcastle United wana kibarua kigumu dhidi ya Paris St Germain ugani St.James Park. Baada ya kushindwa na Wolves siku ya Jumamosi, Pep Guardiola anatarajia ushindi kutoka kwa Man City watakapocheza na RB Leipzig ya Ujerumani.

    Atletico Madrid wataialika Feynoord nayo Porto watakua wenyeji wa vijana wa Xavi Hernandez ,Barcelona.

  • Matokeo ya siku ya Jumatano

    [Picha kwa hisani ya AFC]

    Na Dennis Mungai 

    Mabingwa mara kumi na tatu Real Madrid walipata ushindi wa bao moja kwa bila dhidi ya Union Berlin. Jude Bellingham alifunga bao la pekee mechi ilipokaribia kukamilika na kuipa Los Blancos alama tatu. Arsenal walianza msimu wao kwa kishindo huku wakigaragaza PSV 4-0. Mabao ya Arsenal yakifungwa na Saka, Martin Odegaard, Jesus na Trossard. Inter Milan walitoka sare ya bao moja na Real Sociedad nayo mechi ya Sevilla na Lens kukamilika sawia.

    Napoli walishinda Braga mabao mawili kwa moja, Galatasaray walitoka sare ya mabao mawili dhidi ya Copenhagen na Salzburg walishinda Benfica 2-0. Mechi ya siku ilikua kati ya Bayern Munich na Manchester United. Vijana wa Erik Ten Hag walianza kwa kishindo lakini Bayern walifunga bao la kwanza kupitia Leroy Sane.

    Katika dakika za mwisho Matheus Tel na Casemiro walifungia timu zao lakini mechi ilikamilika Bayern wakipata ushindi wa 4-3. Harry Kane na Serge Gnabry pia walifungia Bavarians. Raundi ya kwanza ya michuano ilikamilika jana na mkondo za mechi za Europa zinatarajiwa kuanza siku ya Alhamisi.

     

  • Matokeo za mechi ya ligi ya mabingwa barani Ulaya

    [Picha kwa hisani ya FC Barcelona]

    Na Dennis Mungai

    Msimu mpya wa ligi kuu ya mabingwa barani Ulaya ulianza jana usiku huku mechi nane zikichezwa. Newcastle United walianza msimu wao dhidi ya AC Milan baada ya kukosa kushiriki michuano hii kwa miaka ishirini. Mechi hiyo ilikamilika sare tasa, kila timu ikitoka na alama moja. Timu nyingine katika kundi lao, Paris St Germain waliishinda Borussia Dortmund kwa mabao mawili kwa sufuri.

    Kwingineko, Barcelona waliiduwaza Royal Antwerp 5-0 huku mabingwa watetezi Manchester City wakitoka nyuma na kuilaza Crvena Zvezda mabao matatu kwa moja. Leipzig walipata ushindi wa mabao matatu kwa moja dhidi ya Young Boys huku Feynoord wakipiga Celtic 2-0. Vigogo wa Ligi kuu nchini Uhispania Atlético Madrid walitoka sare ya bao moja dhidi ya Lazio nayo Porto ikashinda kwa mabao matatu kwa moja walipochuana na Shaktar Donetsk.

    Michuano itaendelea leo usiku huku mechi inayosubiriwa na wengi ikiwa ni kati ya Manchester United dhidi ya Bayern Munich. Vijana wa Erik ten Hag wana masaibu baada ya kumpoteza mchezaji mwingine, Aaron Wan Bissaka, kwa jeraha na kupata kipigo cha 3-1 dhidi ya Brighton siku ya Jumamosi. Timu ya Arsenal inarudi katika michuano hii baada ya miaka saba nje. Wataanza msimu wao dhidi ya PSV ya Uholanzi.

    Mabingwa mara kumi na tatu Real Madrid wataialika Union Berlin ya Ujerumani, mashabiki wa Los Blancos wakipendezwa na kutarajia mengi kutoka kwa mchezaji wao mpya Jude Bellingham. Timu iliyofika fainali msimu uliopita Inter Milan watakabiliana na Real Sociedad huku washindi wa Kombe la Europa msimu uliopita Sevilla wakiialika Lens ugani Ramon Sanchez Pizjuan.

     

  • Matukio na Matokeo Ligi Kuu Nchini Uingereza

    {Picha kwa hisani MyBroadBand}

     

    Na Dennis Mungai

     

    Raundi ya nne ya mechi Ligi kuu nchini Uingereza imekamilika wikendi hii siku ya Jumapili, mechi ya mwisho ikiwa baina ya  Arsenal dhidi ya Manchester United. Mechi yenyewe ilikua ya kusisimua, The Gunners wakipata ushindi wa mabao tatu kwa moja. Declan Rice alifunga bao lake la kwanza kama mchezaji wa Arsenal kisha Gabriel Jesus kufunga la tatu na kuhakikisha ushindi wao. Bao la United lilifungwa na Marcus Rashford kisha Martin Odegaard kusawazisha dakika moja baadaye. Vijana wa Erik Ten Hag sasa wapo katika nafasi ya kumi na moja wakiwa na alama sita huku Arsenal wakiwa na alama kumi.

    Siku ya Jumamosi ilishuhudia wachezaji watatu wakifunga mabao matatu kila moja, ama kwa Kimombo “hat-trick”. Evan Ferguson wa Brighton alifunga mabao matatu kusaidia timu yake kupiga Newcastle 3-1. Erling Haaland alifunga mabao matatu pia na kuzalisha lingine huku vijana wa Pep wakigaragaza Fulham 5-1. Mabao mengine yalifungwa na Nathan Ake na Julian Alvarez. Spurs walishinda Burnley 5-2, Son Heung-Min akicheka na wavu mara tatu huku Romero na James Maddison wakiongezea vijana wa Vincent Kompany masaibu baada ya kupandishwa daraja msimu huu.

    Jurgen Klopp alipata ushindi wa 3-0 katika mechi yake ya mia tatu kama mkufunzi wa Liverpool.  Szoboszlai na Salah walifungia Reds huku difenda wa Aston Villa Matty Cash akijifunga. Crystal Palace walipata ushindi wa mabao matatu kwa mawili dhidi ya Wolves nayo Chelsea walilazwa 1-0 na Nottingham Forest.

    Siku ya Ijumaa West Ham walishinda Luton Town mabao mawili kwa moja, Jarrod Bowen akiendeleza msururu wake wa  kufunga mabao msimu huu. Brentford na Bournemouth walitoka sare ya mabao mawili nayo mechi ya Sheffield United na Everton kumalizika kwa matokeo sawia.  Ligi itachukua mapumziko ya mechi za kitaifa za kirafiki na itaendelea tarehe kumi na sita mwezi huu.

  • Matokeo na Matukio Ligi Kuu Nchini Uingereza

    {Picha kwa hisani ya Bekaboy}

     

    Na Dennis Mungai

    Raundi ya pili za mechi ligi kuu nchini Uingereza ilikamilika jana usiku wakati Arsenal walichuana na Crystal Palace ugani Selhurst Park. Vijana wa Mikel Arteta walipata ushindi wa bao moja kwa bila dhidi ya mahasimu wao wa jadi kupitia penalti iliyofungwa na Martin Odegaard. Beki wa Arsenal Takehiro Tomiyasu alionyeshwa kadi nyekundu lakini the Gunners walishikilia bao lao na kutoka na alama tatu.

    Katika mechi nyingine, Brighton walipata ushindi sawia na ule wa wikendi uliopita kwa kuigaragaza Wolves 4-1  Siku ya Jumamosi. Mabao yao yakifungwa na Solly March, Kaoru Mitoma na Pervis Estupinan. The Seagulls wanaongoza jedwali kwa alama sita na wanaonekana kuwa wakali zaidi licha ya kuuza Alexis Mac Allister na Moises Caicedo. Newcastle United walishindwa na Man City 1-0, bao hilo likifungwa na Julian Alvarez.

    Manchester United walipoteza mechi yao dhidi ya Spurs walipopigwa mabao mawili kwa bila. Mabao ya Spurs yalifungwa na Pape Sarr na mlinzi wa Red Devils Lisandro Martinez alijifunga. Aston Villa waliwaduwaza Everton 4-0 huku mshambuliaji Dominic Calvert Lewin wa Everton akipata jeraha nyingine la uso. Brentford waliendelea kuwashangaza wengi kwa kuipiga Fulham mabao matatu bila jibu na sasa wana alamu sita na kuchukua nafasi ya pili  katika jedwali.

    Mohamed Salah alimpiku Steven Gerrard katika orodha ya wafungaji bora Liverpool kwa kufunga bao katika ushindi wao wa mabao tatu kwa moja dhidi ya Bournemouth. Luis Diaz na Diogo Jota pia walifungia the Reds. Bao la Bournemouth lilifungwa na Antoine Semenyo.

    Siku ya Ijumaa Nottingham Forest ilipata ushindi wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Sheffield United. Mechi ilikaribia kukamilika ikiwa sare lakini mshambuliaji Chris Wood aliingia uwanjani na kutia kimiani bao la ushindi. Raundi ya tatu itaanza siku ya Ijumaa wakati Chelsea itaialika Luton Town ugani Stamford Bridge. Vijana wa Mauricio Pochettino wanatafuta ushindi wao wa kwanza baada ya kupigwa 3-1 na West Ham siku ya Jumapili.

  • LIGI KUU NCHINI UINGEREZA

    Mlinzi wa Manchester United Raphael Varane asherekea bao la pekee katika mechi dhidi ya Wolves siku ya Jumatatu.

    {Picha kwa hisani ya Premier League}

     

    Na Dennis Mungai

     

    Jana usiku Manchester United waliialika Wolverhampton Wanderers ugani Old Trafford kwa mechi ya ufunguzi baina ya timu hizo katika msimu mpya wa 2023/24. Wachezaji wapya wa United Andre Onana na Mason Mount walikua katika kikosi cha kwanza. Mshambuliaji wao mpya  Rasmus Hojlund alipata jeraha kabla ya msimu kuanza hivyo basi alikua nje ya kikosi. Wolves walipata upenyo katika ulinzi wa United na kutengeneza nafasi nyingi za kufunga kupitia wachezaji Matheus Cunha na Pedro Neto lakini hawakupata bao.

    Hatimaye katika kipindi cha pili bao la pekee lilifungwa na mlinzi wa United Raphael Varane baada ya kupewa pasi na Aaron Wan Bissaka. Vijana wa Erik Ten Hag watahisi kutoka na ushindi huo ulikua kibahati kwani Wolves walicheza mchezo bora zaidi katika mechi hiyo. Ushindi huo unakamilisha mechi za ufunguzi katika ligi hiyo.

    Newcastle wanaongoza jedwali kwa alama tatu baada ya kuivuruga Aston Villa 5-1 siku ya Jumamosi, huku Brighton wakichukua nafasi ya pili baada ya kuilaza Luton Town mabao manne kwa moja. Arsenal walianza msimu kwa kuipiga Nottingham Forest mabao mawili kwa moja. Mabingwa watetezi Man City walifungua msimu kwa kuishinda Burnley 3-0. Mfungaji bora Erling Haaland aliendeleza alipoachia msimu uliopita kwa kutia kimiani mabao mawili. Fulham na Crystal Palace walipata ushindi sawa wa bao moja kwa bila dhidi ya Everton na Sheffield United.

    Siku ya Jumapili mechi ya Brentford dhidi ya Spurs ilitoka sare ya mabao mawili huku vijana wa Ange Postecoglou wakianza maisha bila mshambuliaji matata Harry Kane. Mabao ya Spurs yalifungwa na Cristian Romero na Emerson Royal. Pochettino alishika usukani kama kocha wa Chelsea na mechi yake ya kwanza dhidi ya Liverpool ilitoka sare ya bao moja. Luis Diaz alifungia the Reds bao la kwanza kisha mlinzi  mpya wa Chelsea Axel Disasi kusawazishia the Blues dakika chache baadaye.

    Ligi hiyo itaendelea wikendi hii, mechi ya kwanza ikiwa siku ya Ijumaa wakati Nottingham Forest itaialika Sheffield United ugani City Ground.