Author: Abdul Shaban

  • WAPI NJIA NITAPATA?

    Na Abdul Shaban

    Ndugu zangu ahlani, wasahlan jamia
    Nawaombea amani, iweni nanyi daima
    Nimenena kwa vinani, taarifa kuwafika
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?

    Mwenzenu nawambieni, limenikuta gharika
    Chonde chonde sikizeni, nipatapo saidika
    Sitanena kwa uwazi, adui atang’amuza
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?

    Nimo ndani ya bahari, nimezama kwa pupa
    Hali imetahayari, sina hata pa kushika
    Mchana hapapo tuli, usikupo kwachafuka
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?

    Nilifanya sana siri, pale nilipompata
    Nikataka msitiri, shida zake kumputa
    Kumbe ndiye baladhuli, wahida hanayo sifa
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?

    Sikufata desturi, nikajivika upapa
    Sikuskiza shauri, uziwi ulinishika
    Nikajivika makini, kumbe sina maarifa
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?

    Baharini si shwari, nimeloa chapachapa
    Maji chumvi kooni, yaniwasha kwa hakika
    Wadudu wa baharini, nawano wanichonyota
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?

    Nimekuwa maskini, sina hata pakushika
    Kila nikipiga mbizi, maji nayo yanivuta
    Sina cha kujistiri, ngiri nayo yaniliza
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?

    Wapi ndugu majirani, waja wote wanipita
    Mniswamehe jamani, nimejifunza hakika
    Wavuvi na makuhani, kwa pamoya nawaita
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?

    Msiniache jamani, mwenzenu nahangaika
    Nimenena hadharani, mnipe njia kupita
    Nisijepo buriani, nyote mkaumbuka
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?

    Nimenena bila khini, ili nipate ng’amuka
    Yeye kashika mpini, msijepo kwa pupa
    Chukueni tahadhari, sote aso tuzamisha
    Nawauliza jamani, wapi njia nitapata?